Social Icons

Friday, October 11, 2013

MUHIMBILI YATIKISIKA!

Stori: Waandishi Wetu
WIKI moja baada ya gazeti hili kuibua skendo nzito ya uozo ndani yake, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) imetikisika huku viongozi wake wakiweweseka na kutapatapa kujinasua katika kashfa hiyo.
Daktari feki akimwangalia mgonjwa wodini.
RIPOTI YA UOZO
Habari za uhakika zilieleza kuwa patashika imejitokeza baada ya mwandishi wa Global Publishers kujigeuza daktari kisha kufanya kazi kwenye hospitali hiyo kwa siku tatu mfululizo bila kushtukiwa na uongozi wala walinzi na kuibua uozo huo.
Tukio hilo liliripotiwa katika ukurasa wa mbele wa gazeti hili toleo Namba 847 la Oktoba 4-10,2013 iliyopewa kichwa cha habari; KIOJA MUHIMBILI, MWANDISHI GLOBAL AJIFANYA DOKTA MUHIMBILI, AFANYA KAZI ZA UDAKTARI KWA SIKU TATU BILA KUSHTUKIWA.
Katika habari hiyo, mwandishi wetu alisimulia jinsi usalama wa wagonjwa kwenye hospitali hiyo ulivyo mdogo kiasi cha kumuwezesha mtu yeyote ambaye si daktari kuingia wodini akiwa na mavazi ya kidaktari, kuona wagonjwa, kusoma mafaili yao, kuingia chumba cha upasuaji hadi katika ofisi za utawala bila kushtukiwa.
...Akiongea na wagonjwa.
LENGO LILIKUWA KUTOA TAHADHARI
Hata hivyo, lengo la habari hiyo lilikuwa kutoa tahadhari juu ya usalama wa wagonjwa na hospitali nzima ili kusije tokea hatari ya aina yoyote hivyo kuwafanya viongozi wa hospitali hiyo kuchukua hatua kwa kuboresha ulinzi na umakini.
Mara baada ya habari hiyo kuingia mtaani Ijumaa iliyopita na kuibua mshtuko mkubwa, siku mbili baadaye uongozi wa Muhimbili ulituma barua kwenye gazeti hili ukitaka maelezo ya kile kilichoandikwa huku ukihitaji majibu ndani ya siku mbili.
Wakati barua yao ikijibiwa, uongozi huo ulitoa taarifa kwa umma kupitia magazeti mbalimbali ukidai kuwa habari hiyo haikuwa na ukweli na kwamba mwandishi huyo hakufanya kazi za udaktari hivyo gazeti hili linalazimika kuthibitisha ukweli wa kilichoandikwa.
Matukio yote aliyoyafanya mwandishi huyo aliyejifanya dokta yalikuwa yakirekodiwa kwa picha za mnato na video hivyo ushahidi wa habari hiyo mahakamani upo wa kutosha.
...Akiwa ndani ya hospitali.
MASWALI
Taarifa kwa umma iliyotolewa na hospitali hiyo ilieleza kuwa katika habari ya gazeti hili hakuna mahali palipoonesha kuwa mwandishi huyo alifanya kazi ya udaktari jambo lililoibua maswali kwa walioisoma taarifa hiyo ukilinganisha na habari ya kwenye gazeti.
Taarifa ya hospitali hiyo imehoji mambo kadhaa iliyodai kuwa ndiyo majukumu ya daktari ambayo mwandishi wetu hakuweza kuyafanya.
USHAHIDI WA KUMWAGA
‘Daktari’ wetu alifanya mambo kadhaa yanayofanywa na madaktari wa hospitali hiyo ambayo pia yamerekodiwa kama ifuatavyo:
Kwanza, alifanikiwa kuingia katika wodi za Mwaisela na Kibasila na kukagua wagonjwa. Akiwa huko aliuliza maendeleo yao sanjari na kusikiliza matatizo.
..Akikagua vyeti vya wagonjwa.
Pia, akiwa katika mavazi hayo ya kidaktari, aliaminiwa na wagonjwa kiasi cha kupewa kusoma mafaili yao kwenye vyeti vya X-Ray. Tena mgonjwa aliyekuwa na cheti cha X-Ray ni mfungwa.
Pia, ‘dokta’ wa Global Publishers aliweza kushirikiana na wahudumu wengine wa hospitali hiyo kujua ratiba za siku za madaktari na kuingia hadi chumba cha upasuaji.
Ijumaa linaamini kuwa uongozi wa hospitali hiyo ya umma umekurupuka kutoa taarifa kwa kutumia fedha za walipa kodi bila kusoma habari yetu mstari kwa mstari kwani ilifafanua kila kitu.
Mwandishi wetu alifanya vitu hivyo vyote huku akipishana na kusalimiana na madaktari wengine ndani ya hospitali hiyo na kumalizia kwenye Ofisi ya Ofisa Habari, Aminieli Aligaesha ambaye pia alizungumza naye bila kushtukiwa.
WAGONJWA WANASEMAJE?
Wakati hayo yakiendelea huku uongozi ukitaka kujinasua katika kashfa hiyo nzito, gazeti hili liliendelea na uchunguzi wiki hii ndani ya hospitali hiyo ambapo lilizungumza na wagonjwa waliosoma habari hiyo wiki iliyopita kisha wakamwaga maoni yao.
Katika Wodi ya Mwaisela, mmoja wa wagonjwa waliolazwa mwanzoni mwa wiki hii alilieleza gazeti hili kwamba kwa habari hiyo ni dhahiri kuwa kuna uzembe mkubwa ndani ya hospitali hiyo hasa juu ya usalama wa wagonjwa na taasisi kwa jumla.
“Kama hali ndiyo hii, inawezekana mtu hatari akaingia wodini na kujifanya daktari kisha akawachoma sindano ya sumu wagonjwa wote wakafa. Litakuwa ni janga kubwa. Afadhali gazeti limetoa angalizo ili yakitokea ya kutokea watu waseme Gazeti la Ijumaa lilitahadharisha juu ya suala hilo,” alisema.
MKURUGENZI ANG’OLEWE
“Lakini kwa nini tufike huko wakati kuna uwezekano wa kuzuia yasitokee? Kwa kashfa hii, Mkurugenzi wa Muhimbili (Dkt. Marina Njelekela) ang’olewe ili tuokoe hatari hii kwani ameshindwa kazi,” alipendekeza mgonjwa mwingine.
Juu ya habari hiyo, baadhi ya wagonjwa kwenye Wodi ya Kibasila hospitalini hapo walisema kuwa kuna kila sababu ya kuongeza umakini hasa suala la kutambuana ili kuziba mwanya kwa mtu mwingine mwenye nia mbaya na asiye daktari kufanya hujuma yoyote.
“Hapa kuna tatizo la umakini hasa suala la vitambulisho vya kutambuana. Kwa hali ilivyokuwa ilikuwa rahisi kwa mtu yeyote kuvaa koti jeupe na kubeba kipimo kisha kuingia wodini kwa heshima zote bila kuzuiliwa popote.
“Uongozi ulipaswa kulishughulikia suala hilo badala ya kuanza kutumia nguvu kubwa kukanusha habari wakati ukweli ni kwamba hali ya usalama Muhimbili ni tete,” alisema mmoja wa wagonjwa wodini hapo na kuongeza:
“Unajua taasisi nyingi za serikali hawapendi kukosolewa au kuambiwa ukweli, wanapenda kusifiwa tu jambo ambalo haliwezekani kwani hata siku hazifanani. Hapa lazima Waziri wa Afya (na Ustawi wa Jamii, Dkt. Hussein Mwinyi) achukue hatua mara moja ili hii ishu isipite hivihivi.
“Penye hatari lazima pawe na tahadhari, watu wajipange, wawe makini zaidi, siyo kwamba hawapo makini lakini ni vema umakini ukaongezeka hasa kwa kipindi tulichonacho cha tishio la ugaidi.”
MSISITIZO
Dawati la Gazeti la Ijumaa linasisitiza kuwa lengo la habari ile halikuwa baya bali ni kupima ulinzi na umakini wa hospitali yetu, kwa vile ndiyo kubwa na inayotegemewa na umma. Hii ni hospitali ya Watanzania, ni jukumu letu kusaidia kuwakumbusha waliopewa dhamana kuwa makini.
Tunawaomba viongozi wa Muhimbili kuchukua habari yetu kama changamoto, kama walivyofanya watu wa Mlimani City na Uwanja wa Taifa ambao baada ya sisi kuandika habari za kueleza upungufu wa ulinzi katika maeneo hayo, mara moja walichukua hatua.
IJUMAA KUPELEKA RIPOTI KWA JK
Endapo uongozi wa Muhimbili utaendelea kutumia fedha za walipa kodi kukanusha ukweli huu kwa kusambaza ripoti kwenye vyombo vya habari,  gazeti hili lipo tayari kupeleka video yenye tukio zima kwa Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete kwa hatua muafaka.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

No comments:

Post a Comment

 

for more information call us

+255718953088
-------or-------
+255784953088
*email*
innocentfabian@gmail.com
THANKS

quote of the day

"Don't criticize me simply because I am different. Understand me, and you will most likely appreciate my difference and criticize your variance."