HAPA
 ndiyo sehemu pekee ya kupanua mawazo na kukuza ubongo wako juu ya mambo
 yanayohusu uhusiano na mapenzi. Kama ni mara yako ya kwanza kuanza 
kupitia ukurasa huu, umekutana na kona muhimu sana. Huna cha kupoteza. 
Utajengeka kila siku.
Rafiki
 zangu, leo nimekuja na mada mpya baada ya kuhitimisha ile ya wiki 
iliyopita. Nina imani kuna mengi mliyojifunza. Mada ya leo inatokana na 
maswali mengi ya aina moja niliyoyapata kwa muda mrefu kutoka kwa 
wasomaji mbalimbali.
Hebu
 msikie huyu: “Pole na kazi kaka Shaluwa, kuna kaka nawasiliana naye. 
Kiukweli tumezoeana sana, juzi hapa amesema eti ananipenda na anataka 
kunioa. Mimi nipo Mbeya, yeye anaishi Dar es Salaam.
“Hatujawahi
 kuonana, zaidi ya kuzungumza kwa njia ya simu tu. Nilifahamiana naye 
baada ya kukosea namba, ndipo tukakubaliana kuwa marafiki. Tafadhali 
naomba msaada wako maana ninachanganyikiwa kabisa. Ni kweli 
ananipenda?”. 
Kilio
 kama hicho nilikipata pia kutoka kwa msomaji mmoja ambaye naye 
sitachapa jina lake gazetini. Huyu alisema: “Nimekutana na rafiki kwenye
 Facebook, tunawasiliana mara kwa mara, ninahisi kumpenda huyo msichana.
 Naye ana kila dalili za kunipenda, tatizo sijaanza tu kumweleza. Hivi, 
inawezekana kweli tukapendana kabla ya kuonana?”
Bila
 shaka kuna picha umeipata kupitia maswali ya wasomaji hao wawili. 
Niliwaahidi kuandika mada gazetini ambapo ndipo wangepata majibu yao. 
Je, wewe upo kwenye kundi gani?
Umewahi
 kukutana na jambo hilo? Unadhani unaweza kumpenda mtu kabla ya kukutana
 naye? Sauti pekee inaweza kumfanya mtu ampende mwenzake kwa dhati na 
mapenzi yao yakadumu? Twende tukajifunze.
INAWEZEKANA?
Hili
 ni jambo la kwanza linalotakiwa kupatiwa majibu kabla ya kuendelea na 
mada hii. Huu ni mtazamo hasi. Jibu kwa kifupi tu ni haiwezekani. 
Utawezaje kumpenda mtu ambaye hujamuona?
Misingi
 ya kumpenda mwingine ikoje? Kanuni zipo wazi; KUPENDA ndiyo jambo la 
kwanza, ambapo ukweli ni kwamba huanza na kutamani, sasa itawezekanaje 
kumtamani mtu ambaye hujawahi kukutana naye?
Baada
 ya kupenda, kuna mambo mengine ya msingi ambayo ni muhimu kuzingatiwa 
ili kujihakikishia kwamba uliyempata ni mwenzi sahihi. Kuna suala la 
kuchunguzana tabia n.k, yote haya yatawezekana vipi kufanyika kabla ya 
kukutana?
Najua
 ni wengi wamekumbana na hili ninalolizungumzia hapa, unashindwa cha 
kufanya na kubaki gizani. Leo utarudi kwenye mwanga! Unajua chanzo cha 
yote hayo ni nini? Twende kwenye kipengele kinachofuata.
HUANZA HIVI...
Chanzo
 kikuu cha udanganyifu huu wa mapenzi huwa ni vyombo vya mawasiliano. 
Mfano mtu amepiga simu amekosea namba...mara anaanza ‘uko wapi? Haina 
neno, tunaweza kuwa marafiki?’
Mazoea
 yakizidi, kila mmoja huanza kumwuliza mwenzake vitu anavyopendelea na 
mambo mengine. Baadaye wanatongozana! Huelezana mambo mengi sana na 
ahadi nyingi wakiamini kwamba wanapendana kwa dhati!
MAPENZI YA HISIA
Kimsingi
 sababu ya haya yote ni hisia tu. Njia ya mawasiliano inaweza kukoleza 
au kuimarisha uhusiano ambao tayari upo. Mfano kama unaishi Moshi na 
mpenzi wako yupo Mwanza, mnaweza kuboresha uhusiano wenu kwa kuwasiliana
 kwa njia ya simu, waraka pepe na mitandao ya kijamii.
Kinachotokea
 kwa marafiki wapya ambao wanahisi tayari ni wapenzi na wanapendana ni 
zile hisia za ndani zinazowaingia wakati wa mawasiliano yao. Pengine 
walianza kuzungumzia mambo ya mapenzi na kujikuta wakitamani kuwa 
karibu.
Jambo
 kubwa zaidi ni kwamba mhusika hutawaliwa zaidi na hisia, maana kwa 
sababu hawafahamiani, watakuwa wanauliza; ‘Wewe ukoje? Mrefu, mfupi, 
mwembamba, mnene au?’ halafu mwenzake atamjibu, ‘mrefu kiasi, si mnene 
sana, kifupi nina umbo namba nane...navutia na ni maji ya kunde’. 
Kifupi
 mtu anaweza kujielezea vyovyote atakavyo, hivyo kumfanya mwenzake 
amtengeneze ajuavyo kichwani mwake na kujihakikishia kwamba anampenda 
kwa dhati mwenzake kumbe anajidanganya!
TABIA BANDIA
Mbaya
 zaidi ni kwamba, wakati wapenzi hawa wanaojidanganya wakiendelea 
kuwasiliana si rahisi kujuana vizuri kitabia kwa sababu wengi huonesha 
tabia bandia. Mambo yao ya ndani wanayaficha kwa nguvu na kuonesha mema 
tu.
Hapo ndipo mwanzo wa penzi feki kwa kudanganyika na tabia za kutengeneza.
HULKA MBAYA
Kuna
 wengine ni tabia zao za asili. Amezoea kupata wapenzi kwa kupitia 
kwenye simu na mitandao ya kijamii. Usishangae kuna wengine wanapiga 
namba hata wasizozijua, akikutana na mtu wa jinsia tofauti na yake, 
anaanza mambo yake. Akimaliza haja zake anakuacha!
ACHA KUJIDANGANYA
Ni
 vizuri sasa ukatoka kwenye ulimwengu wa giza na kurudi kwenye ulimwengu
 unaonekana. Kwa hakika ni vigumu sana kumpenda mtu ambaye hujamuona, 
labda kama unataka kucheza na muda wako.
Wako
 anakuja, vuta subira ukifanya mambo yako kwa usahihi. Usijidanganye na 
matapeli wa mapenzi. Wapo ambao wanafanikiwa kuingia kwenye mapenzi 
lakini mwisho wao hauwi wenye mafanikio.
Penzi
 la dhati hubebwa na vitu vingi sana, ukiachana na UPENDO kuna suala la 
tabia na mengine mengi ambayo huwezi kuyajua kwa njia ya kuwasiliana 
pekee. Utajihakikisha umempenda kwa kumtengeneza kichwani mwako, mwisho 
wa siku unakutana na mtu ambaye yupo tofauti na mawazo yako, itakuwaje 
hapo?
Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Mambo ya Mapenzi anayeandikia magazeti ya 
Global Publishers. Ameandika vitabu vya True Love, Let’s Talk About Love
 na Who is your Valentine? vilivyopo mitaani.
KWA HABARI ZAIDI ZA MAHUSIANO NA NYINGINE INGIA:
                    
 TOA MAONI YAKO HAPA CHINI