Social Icons

Wednesday, May 15, 2013

BARUA NZITO : USTAA ULIONAO LEO UKUTENGENEZEE UZEE MZURI!

KWENU,
Wasanii mnaong’aa katika sanaa mbalimbali nchini. Ninafurahi kuwasiliana nanyi tena kwa wakati mmoja baada ya kuachana muda mrefu uliopita. Naamini mpo sawa na michakato ya kusaka mkate wa kila siku inaendelea vyema kabisa.
Kama ndivyo, ndiyo furaha kwangu. Nazungumza nanyi mastaa katika fani mbalimbali Bongo. Inawezekana wewe ni mwanamuziki, mwanasoka, mtangazaji, mchoraji, mchongaji, mwanamitindo au msanii wa filamu.
Nyota yako kwa sasa inang’aa na kila unapopita unakubalika. Ni jambo la kujivunia sana. Heshima yako ni kubwa kupitia sanaa yako. Inawezekana wewe ni mtunzi wa vitabu na unakubalika sana kwa kazi yako ambayo inakuingizia fedha nyingi.
Hongereni wote kwa pamoja. Pamoja na yote hayo, yapo mambo ya msingi ambayo nataka kuwashauri ili muweze kubaki kileleni siku zote na  mwisho wa siku muwe na uzee mzuri usiosababisha kero kwa wengine. Mmenipata ndugu zangu?
TAFUTA KUWA NAMBA MOJA
Ukiwa kama staa, usijisahau katika nafasi uliyonayo na kudhani labda utaendelea kuwa hapo siku zote. Dunia inabadilika na ushindani kwenye sanaa yoyote ni mkubwa. Usibweteke kwa unachopata leo ukaona kinatosha.
Umiza kichwa zaidi ili uwe/uendelee kuwa namba moja. Kuwa mbunifu zaidi na endelea kujifunza ili uwe staa mkubwa nchini. Chipukizi wengi wanakuja nyuma yako, ukilegeza kidogo tu unaachwa!
KIMATAIFA ZAIDI
Baada ya kujihakikishia kwamba umeshika nafasi ya juu Bongo, unatakiwa kupanua zaidi ubongo wako na kujifunza ili uwe wa kimataifa. Huwezi kubaki hapohapo na ukaendelea kujiona wewe ni staa.
Thubutu! Marehemu Steven Kanumba alionesha mwanzo mzuri. Wengine wanaofuata nyayo zake ni Lucy Komba, Hashim Kambi, Wema Sepetu na baadhi ya wanamitindo na wacheza soka ambao wanajaribu kutafuta soko la kimataifa.
ANZISHA MIRADI
Pamoja na mafanikio makubwa ya kimataifa, huwezi kujiita staa na kujivunia kama hutawekeza katika miradi. Kama nilivyosema awali, chipukizi wengi wanakuja nyuma yako na wanaweza kukushusha wakati wowote.
Ili kuepuka hilo ni vyema kutazama kesho yako – siku ukishuka na kushindwa kufurukuta kwenye sanaa. Anzisha miradi ambayo itakusaidia. Fungua biashara au kampuni mbalimbali kwa kutumia lebo ya jina lako ambalo tayari lipo juu.
Siku zijazo ukishastaafu, hutakuwa na dhiki wala kuomba misaada. Mifano ipo mingi tu. Wapo mastaa wengi wa zamani, sasa hivi wanateseka. Juzi tu, Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Mhe. Amos Makalla alijibu hoja bungeni, Dodoma akisema kwamba, serikali haina utaratibu wa kuwasaidia wanasoka pindi wanapostaafu.
Umeona kazi hiyo?
MIFANO IKO WAZI
Pongezi kwa mastaa ambao wameshtuka mapema na kujiwekea misingi ya baadaye. Wapo ambao wamejenga nyumba, wamefungua kampuni na mambo mengine mazuri ambayo yataendelea kubaki hata kama ustaa utatoweka.
Wapo wengi lakini hapa nakutajia wachache kama Jide, AY, Profesa Jay, Izzo Business, Jafarai, Juma Nature, H – Baba, Dully Sykes, Mike T na Chegge (Bongo Fleva), JB, Ray, Pastor Myamba, Wema Sepetu, King Majuto, Aunt Ezekiel (Bongo Movies), Aboubakar Sadiq, B12, Harris Kapiga, Dida (watangazaji) na Kaseja na Ngassa (soka).
Hawa wawe mfano kwako na wakupe nguvu ya kuandaa maisha yako baada ya ustaa wako kushuka. Kumbuka unaweza kuendelea kuishi kistaa hata baada ya kuwa nje ya gemu. Uamuzi upo mikononi mwako.
Yuleyule,
Mkweli daima,
.................
Joseph Shaluwa
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

No comments:

Post a Comment

 

for more information call us

+255718953088
-------or-------
+255784953088
*email*
innocentfabian@gmail.com
THANKS

quote of the day

"Don't criticize me simply because I am different. Understand me, and you will most likely appreciate my difference and criticize your variance."